Lebo

Jumatatu, 15 Juni 2015

EXCLUSIVE...Usichokijua kuhusu laana ya dhahabu Mkoani Geita!

Wachimbaji na wafanyakazi wengine katika eneo la Mgusu, hakuna matumizi yoyote yale ya vifaa vya kujikinga na sumu ya mercury. Ni wakati muafaka kwa wadau kujitokeza kutoa elimu ili watu hawa wajue madhara ya mercury na namna ya kujikinga.

 Yapo mambo mengi nchini kwetu ambayo kama hayatabadilishwa kwa namna moja u nyingine basi madhara makubwa hayazuiliki siku za usoni. Unapokuwa mikoa ya mbali mathalani Mbeya, Dar, Morogoro, Dodoma n.k kisha ukapata simulizi kwa jinsi ambavyo Mkoa wa Geita umebarikiwa kwa madini aina ya dhahabu, bila shaka utajenga picha fulani hivi kubwa kichwani kwa kulinganisha na uthamani wa madini yenyewe.

 
Awali, utajiaminisha kwamba mkoa wa Geita hauna shida kubwa ya huduma za kijamii hivyo maji, umeme, barabara, hospitali na shule si masuala ya watu kuyalalamikia. Pia utajiaminisha kuwa tatizo la ajira laweza kuwa dogo kwa maana pato la dhahabu laweza kuchagiza sekta nyingine mathalani kilimo na viwanda. Lakini yote hayo ni matamanio ya kifikra tu japokuwa hata wakazi wa mkoa huo wangependa hali iwe hivyo lakini haijawezekana tena kwa miaka lukuki.

Kwa kuangazia kidogo suala la maji bado ni shida, Geita mjini hakuna maji safi na salama yaliyosambazwa kwa umma japokuwa kwa sasa kuna maandalizi ya kufanya hivyo. Utakutana na baadhi ya vijana wakikokota matoroli huku na kule wakiuza maji ya kisima. Kuhusu ajira tatizo bado kubwa kwa maana hakuna hata kiwanda kimoja chenye uwezo wa kuajiri vijana wengi nje ya mgodi wa GGM na migodi mingine midogo midogo, hofu ya wakaaji ni ikiwa migodi hii itafungwa pindi dhahabu ikiisha.

ENEO LA WACHIMBAJI WADOGO

Wakati kuna hoja nyingi kuhusu kujiajiri na kuzitumia rasilimali zilizopo, wachimbaji wadogo mkoani Geita hawana amani. Kijana mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Pius Malila (Amegoma kupigwa picha) amesema wanafukuzwa hovyo kama wakimbizi katika nchi yao. Amesema, "Hatutengewi maeneo, na hata kwa jitihada zetu tukipata sehemu panapohila basi askari wanakuja na kutufukuza kisha eneo hilo anakabidhiwa mwekezaji, waziri mkuu alituahidi kwamba tutapewa hati za viwanja vya machimbo lakini matumaini na madogo na tunaelekea kukata tamaa".

Ili mradi makala hii haijalenga kuwazungumzia wachimbaji wadogo na kukosa dhamana ya maeneo, ningependa niweke wazi kwamba hakuna uwezeshaji wa maana uliofanyika mkoani Geita kwa lengo la kuwainua wachimbaji wadogo mpaka sasa ambapo wenye mamlaka waweza kujivunia. Kwa utafiti niliofanya, nimegundua kuna wimbi kubwa la vijana wanaojihusisha na uchimab

Vijana wengi hawana ajira baada ya machimbo mengi kufungwa kwasababu za kiusalama, afya au hata urasimu. Lakini hata wale wanao endelea na uchimbaji hali ikoje?

1/KUNA USALAMA?

2/KUNA TIJA?

3/KUNA UBINADAMU?.

Nimetembelea katika eneo la machimbo la Nyakabale na Mgusu katika halmashauri ya mji wa Geita na hali iko hivi;

 
Hatua ya awali pale inapogundulika dhahabu ni kusafisha mazingira, hivyo kwa kuwa hapo unapoona palikuwa ni eneo la msitu basi kilichobaki ni kuni.
Wanyama hawa huishi kwa amani panapo uoto wa asili lakini kwa kuangalia ile picha ya kwanza utagundua kwamba kizazi kijacho kitawafahamu wanyama hawa kwa kutembelea makumbusho tu.

Bila shaka umejionea mwenyewe kuhusu kule tunakoelekea hivyo endelea kunifuatilia.
Ukitazama rangi ya maji hayo hapo juu utagundua kwamba si salama wala haifai kwa binadamu kunywa, kunawa au hata kutembea peku peku kwa maana maji hayo yamechanganyikana na kemikali aina ya zebaki inayodhuru ngozi na seli hai zake. Lakini maji hayo yametoka wapi?
Najua una hamu ya kutaka kujua nakupeleka wapi lakini usiwe na haraka, kwenye picha hii utaona binadamu na wanyama wanatumia maji hayo hayo yenye kemikali huku wengine wakiyatumia hata kwa kupikia chakula.
Eneo hili ni maarufu kama sehemu ya kuoshea dhahabu na wachimbaji wadogo hulitumia eneo hili katika moja ya hatua ya kukamilisha mchakato wa kutengeneza dhahabu. Maji yanayotoka hapo hayana mkondo maalumu licha ya kujaa sumu hivyo hutiririka kwenye hicho kimto ambacho watu huyatumia maji yake kwa kupikia, kuoga na kunywesha mifugo.

Wakati kukiwa na kelele nyingi kuhusu kupiga vita ajira kwa watoto na kuhakikisha mtoto wa kike anasoma, hali sivyo kwa watu masikini mkoani Geita. Mama huyo anaponda mawe ya dhahabu sambamba na mwanae katika harakati za kujipatia mkate wa kila siku. Pahala pengine kuna watoto wadogo kuzidi huyo mtoto wa kike. Wachimbaji wadogo hawana mitaji hivyo hawana mashine za kusaga mawe badala yake kazi hiyo hufanywa na binadamu.
Kina mama wakimaliza kupondaponda mawe, zamu inahamia kwa vijana hawa ambao ni wachenjuaji wa dhahabu. Wanaosha kisha mchakato mwningine utaendelea. Hapa ni hela kwanza, afya na usalama vitafuata maana hawana namna.
Usidhani hapo wanaume wazima wanaota moto lahasha, wanachoma dhahabu ikiwa ni moja kati ya maandalizi kabla ya kuiuza kwa kudalaliwa tena kwa bei anayopanga mnunuaji. Ndiyo, sasa kama utagoma kuwauzia si ajabu ukaundiwa genge la watu wakakuvamia na kukuua kisha wakaondoka na mali.
Shughuli ya uchimbaji dhahabu imekuwa ngumu, hakuna maeneo maalumu kwa ajili ya wachimbaji wadogo. Kijana huyu akiliwakilisha kundi jingine kubwa la vijana wameamua kujiingiza kwenye shughuli nyingine. Yeye mwenyewe amesema, "hatuwezi kuiba, siku kwenye magwangala kuna 'MAFIDI', wakikukamata lazima wakuache kilema. Tumeamua kufanya shughuli ya uchomaji mkaa. Maliasili wakija tunakimbizana nao hivyo hivyo. Hakuna utajiri humu kwenye mikaa lakini hatuna namna maana dhahabu ya Geita sasa ina wenyewe".
Pamoja na mambo mengine mengi, hakuna matumaini ya wananchi kunufaika moja kwa moja na rasilimali zao. Nisikuchoshe sana, makala ijayo itazungumzia athari ya zebaki kwa afya ya binadamu wakiwemo watoto wadogo kama hawa hapa.

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni