Lebo

Jumamosi, 27 Juni 2015

Mhe .Joseph mbilinyi alipolia Bungeni jana

Mhe.Joseph Mbilinyi akiwa na mzazi mwenza Faiza Ally sambamba na mtoto wao kabla ya migogoro kuanza

Jana ilikuwa siku ya aina yake kwa msanii Faiza Ally na mzazi mwenzake, Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi ‘Sugu’. Wakati Faiza akimwaga chozi katika chumba cha habari katika gazeti la Mwananchi alipofika kutoa ujumbe wa kuomba radhi kutokana na vazi la kitenge lenye kambakamba alilovaa siku ya Tamasha la Tuzo za Muziki za Kilimanjaro, Sugu alimwaga chozi bungeni Dodoma alipowataka wabunge wasijadili mambo yake ya faragha.
 Sugu 11

Faiza akiwa amevalia baibui na kufunika kichwa kwa hijabu, alieleza kwamba anajutia kutokana na kuvaa vazi lililoonyesha sehemu kubwa ya makalio yake alilodhani ulikuwa ubunifu. Mrejesho alioupata kuzomewa na jamii na picha zake kusambazwa kwenye mitandao ya kijamii aligundua amefanya kosa.

Pigo la pili, ambalo limemjeruhi vibaya moyoni ni mzazi mwenzake, Sugu kufungua kesi katika Mahakama ya Mwanzo ya Sinza iliyompa haki ya kukaa na mtoto wao kwa madai mama yake kukosa maadili.

Hivi sasa Faiza anaona dunia imemwelemea anajuta na ameapa kutorudia tena kosa hilo. “Siwezi kurudia kosa, nitakuwa makini zaidi katika mavazi yangu,” alisema msanii huyo, huku akitokwa machozi alipozungumza jana na mwandishi wa habari hizi kwenye ofisi za gazeti hili zilizopo Tabata Relini, Dar es Salaam.

Mwanadada huyo aliyewahi kuwa mrembo wa Tabata namba tatu katika mashindano ya mwaka 2005 na ambaye hujishughulisha na utayarishaji filamu, aliomba radhi kwa jamii kutokana na utovu wa maadili aliouonyesha siku ya tuzo hizo na bado anaomba wamsamehe.

“Wasanii wengi ni wabunifu na hufanya mambo kwa nia ya kufurahisha mashabiki kama ambavyo amekuwa akifanya Joti kuvaa nguo za kike na kupaka rangi ya mdomo, hivyo mavazi yangu yalikuwa na lengo la kutoka tofauti mbele za mashabiki wangu, lakini kwa yaliyonikuta hasa kwenye vazi la Kili niliomba msamaha kwa jamii na bado naomba wanisamehe,” alisema Faiza.

Hata hivyo, hilo la mzazi mwenzake kupewa haki ya kisheria na mahakama kumchukua mtoto wao mwenye umri wa miaka miwili na miezi minane, kwa madai kadhaa ikiwamo ya uvaaji usiokuwa na staha, ni jeraha kubwa lililomfanya apite kwenye vyombo vya habari kupaza sauti ya kuomba radhi.

Sakata hilo pia limetua bungeni na baadhi ya wabunge wanawake walimlaumu Sugu wakidai kampora mtoto mzazi mwenzake kwa vile ni mnyonge, lakini jana mbunge huyo, aliyewahi kutamba nchini na muziki wa Hip Hop alitoa ufafanuzi wa kina na kuwataka wabunge wasiingilie maisha yake ya faragha.

“Wabunge tuliomo humu ndani, baadhi wametumia madaraka yao vibaya katika kuwanyanyasa wanawake. Ninasema haya kwa sababu nina ushahidi. Tuna mbunge mwenzetu amemnyanyasa mwanamke mwenzetu, ameenda kutumia siku moja mahakamani kumnyang’anya mtoto wa miaka miwili, kitu ambacho kwa kweli wanaume waangalie namna ya kuwaenzi na kuwaheshimu wanawake hasa katika suala la kulea watoto. Ni mbunge kutoka Chadema kama Chadema wanathamini utu wa mwanamke wangemshauri mbunge mwenzao,” alisema juzi mbunge wa viti maalumu (CCM), Martha Mlata.

Hata hivyo, jana Sugu alijibu kwa uzito akieleza taratibu alizotumia kufungua kesi mahakamani, uamuzi ulivyotolewa na namna alivyomwacha kwanza mtoto kwa mama yake yafanyike majadiliano ya kifamilia.

“Kwa taarifa tu pamoja na mahakama kunipa haki, mtoto bado yuko kwa mama yake kwa sababu mimi ni mstaarabu, nimetoa nafasi ili majadiliano ya kifamilia yafanyike. Naomba mjadala huu usiendelee zaidi ya hapa,” alisema Sugu ambaye alionekana akifuta machozi akisikitishwa suala hilo kuzua mjadala bungeni.
SOURCE; mwananchi newspaper

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni