Lebo

Jumamosi, 30 Mei 2015

Lowassa ameshindwa kujitenga na ufisadi wa Richmond huko Arusha.

Katika siasa kuna kitu kinaitwa ncha ya maslahi ya watu au kwa kimombo, 'the angle of people's interests'. Kwa muda mrefu tangu alipojiuzulu uwaziri mkuu kutokana na kashfa ya kampuni hewa ya ufuaji umeme almaarufu RICHMOND, Mhe.Edward Lowassa ambaye pia ni mbunge wa Monduli aligeuka bubu na alikuwa hasikiki kabisa mpaka mwaka 2012 alipoonekana tena jukwaani Arumeru Mashariki alipokuwa akimpigia kampeni aliyekuwa mgombea ubunge kwa tiketi ya CCM ndugu Sioi Sumari. Katika uchaguzi huo CCM walibwaga chini na Mhe.Joshua Nassari (CHADEMA) alichaguliwa kuwa mbunge.
Pamoja na mambo mengine, kwa muda mrefu kumekuwa na sintofahamu kuhusu kipi ni kweli kuhusiana na Mhe.Lowassa na ufisadi wa RICHMOND. Kutokana na taarifa za awali kwamba Mhe.Edward Lowassa atatangaza nia leo, wadau wa habari, wachambuzi wa mambo ya kisiasa na wananchi wa kawaida walikuwa chonjo kutaka kujua kama ni kweli Mhe.Lowassa ataeleza ukweli kuhusu uhusika wake katika sakata la RICHMOND lakini jambo hilo hajalizungumzia kabisa.

Mhe.Edward Lowassa (mwenye shati la kijani na mvi) akisalimiana na wapambe wake baada ya kutangaza nia rasmi katika uwanja wa Amri Abeid.

Jisomee mwenyewe hapo chini sehemu ya hotuba yake uone kama kuna pahala amezungumzia sakata la RICHMOND au kuwa na lengo la kupiga vita ufisadi;

"Mimi, baada ya kutafakari kwa kina changamoto tulizo nazo na matarajio na matumaini waliyo nayo Watanzania, naamini kwamba Uongozi imara unaolenga kujenga Taifa imara unapaswa kuwa na dira yenye malengo yafuatayo:

-    Kuimarisha Muungano wetu kwa kuyashughulikia yanayotutenganisha na kuyafanyia kazi ili yasivuruge yale yanayotuunganisha ambayo ni mengi zaidi na makubwa zaidi.

-    Kushughulikia matumizi mabaya ya siasa za udini na ukabila kwa kuimarisha siasa zilizoshiba uzalendo na zenye kutuelekeza kwenye Utanzania wetu.

-    Kujenga uchumi imara na wa kisasa, na ambao ni shirikishi unaomnufaisha kila Mtanzania aliyeko mjini au kijijini. Tunapaswa kubadili hali tuliyo nayo sasa ambapo Kilimo kinaonekana kama kimesahauliwa na wakulima wetu wanaonekana wanakata tamaa.
 
Wafugaji na wavuvi nao wanahisi sekta zao hazijapewa umuhimu unaostahiki. Tunahitaji kuondokana na hali iliyopo sasa ya kuwa Taifa linalouza malighafi na badala yake kuwa Taifa linalosindika na kusarifu mazao na kutengeneza wenyewe bidhaa zitokanazo na malighafi yake. 
 
Ndani ya miaka mitano ijayo tutahakikishatunaiondolea Tanzania sifa ya kusafirisha malighafi na badala yake kusindika mazao yanayozalishwa hapa nchini kama pamba, kahawa, chai na korosho na kuyaongezea thamani (value addition).Mkakati huu utazalisha ajira nyingi na kuongeza mapato ya fedha za kigeni nchini.
 
 Tunahitaji kujielekeza kwenye kujenga viwanda na kuleta ajira. Tuna vivutio vingi sana vya utalii lakini bado Tanzania inapitwa na nchi kama Afrika Kusini katika kuingiza idadi kubwa ya watalii.
 
 Kwa nini nchi kama Dubai iweze kuvutia watalii kwa mamilioni na Tanzania tushindwe? Tunapaswa kukabiliana kikamilifu na hisia zilizopo miongoni mwa wananchi kwamba Tanzania hainufaiki ipasavyo na utajiri wa rasilimali zake nyingi ilizo nazo. 
 
Tutajipanga zaidi kuhakikisha tunanufaika kama nchi na rasilimali zetu kama madini na gesi asilia. Hii ndio Safari ya Matumaini

-    Kukuza kipato cha wananchi na kunyanyua hali za maisha ya watu wetu. Tunapaswa kuhakikisha kuwa ukuaji wa uchumi tunaouzungumzia unamnufaisha Mtanzania aliyeko mjini au kijijini na kwamba hali za Watanzania wa matabaka yote zinanyanyuka na kwamba wanaridhika na kuuona uhalisi wa ukuaji wa maendeleo tunayoyazungumzia.

-    Kuondokana na sifa mbaya ya kuwa Taifa ombaomba. Kwa wingi wa rasilimali tulizo nazo na neema ya ardhi, maziwa, mito na bahari Tanzania tuna kila sababu ya kuacha kuwa ‘bakuli la ombaomba’ na badala yake kuwa ‘mkoba wa neema’ katika Afrika.We can transform our nation from being the begging bowl to become the bread basket of Africa.

- Kujenga mfumo mpya wa elimu unaojielekeza kuwatayarisha vijana wetu waweze kuajirika, kujiajiri na kushindana katika soko la ajira. 
 
Tumepiga hatua kadhaa katika elimu lakini kiwango cha elimu bado ni hafifu. Pamoja na kuwa na shahada (degrees), bado wahitimu wetu hawawezi kushindana kwenye soko la ajira. 
 
Wakati tunazungumzia kuunganisha soko la ajira katika Afrika Mashariki,hatuna budi kujikita kubadili mfumo wetu wa elimu na kuuelekeza kwenye mafunzo ya ufundi na stadi yanayowajenga wahitimu wetu kuwa wabunifu na wenye kujiamini katika kukabiliana na changamoto za maendeleo duniani.

-    Kuhakikisha tunakabiliana ipasavyo na kulipunguza kwa kiasi kikubwa kama si kulimaliza kabisa tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama. Ni jambo la kusikitisha kwamba tumezungukwa na mito na maziwa lakini bado watu wetu hawana maji ya kunywa hata ndani ya Dar es Salaam.

-    Kujenga na kusimamia mfumo imara wa kutekeleza sera na sheria tunazozitunga na kuzipitisha kwa lengo la kumtumikia Mtanzania na kumjengea uwezo wa kubadili maisha yake ili tuweze kwenda sambamba na viwango vya kimataifa. Tanzania imepata sera na sheria nzuri sana lakini utekelezaji wake umekuwa hafifu. 
 
Tumekuwa wepesi wa kutunga sera na sheria lakini wazito mno wa kuzitekeleza na kuzisimamia. Uongozi imara wenye kulenga ujenzi wa Taifa imara utahakikisha tunakuwa mfano wa utekelezaji wa sera na sheria tulizo nazo na mpya zitakazotungwa kukabiliana na malengo tuliyojiwekea.

Mambo haya niliyoyaeleza hapa ndiyo yatakayokuwa msingi mkuu wa utendaji wa Serikali nitakayoiongoza pale nitakapopewa ridhaa ya kubeba bendera ya CCM katika nafasi ya Urais na pia nitakapopewa ridhaa ya kuliongoza Taifa letu kupitia uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

Ramani  ya  Uongozi  Imara  Ninaouamini 9 Leadership Roadmap)
Kama nilivyotangulia kusema, kazi ya kuongoza nchi si lelemama na hasa unapoongozwa na dhamira ya dhati na msukumo wa ndani ya nafsi unaojielekeza kubadilisha maisha ya wananchi wenzako waliokuamini uwaongoze. Kwa vyovyote vile, hiyo haiwezi kuwa kazi ya mtu mmoja. Ni kazi ya pamoja.
 
 Lakini ili muweze kufanya kazi kama timu moja iliyojipanga kisawasawa kuleta mabadiliko yanayohitajika na ili muweze kweli kutoa Uongozi imara unaojikita kujenga Taifa imara hapana budi kiongozi mkuu anayeongoza timu hiyo aweke ramani anayokusudia kuifuata katika kutoa uongoziimara anaoukusudia yaani ‘Leadership Roadmap’.

Pamoja na kuwa sehemu ya uongozi huko nyuma, kutakuwa na maamuzi na matumaini mapya. Ramani ya uongozi imaraninayokusudia kuutoa kwa wenzangu na ambayo nitaitumia kuiongoza timu yangu katika kuwatumikia Watanzania wenzangu itajikita katika maeneo yafuatayo:

1. Kurejea kwenye Katiba katika kuainisha nia, dhamira na malengo yetu ya kujenga jamii inayozingatia misingi ya demokrasia, udugu na amani. Muhimu katika hili ni kukemea tabia mbaya zinazochochea mfarakano katika jamii kama vile matumizi mabaya ya siasa za udini na ukabila.
 
Aidha moja ya misingi muhimu ya Katiba ni Muungano wetu. Itakuwa dhamira yangu kuimarisha misingi ya Muungano pamoja na udugu wa damu nahistoria ya ushirikiano iliyojengwa na waasisi wetu, Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Hayati Sheikh Amri Abeid Karume na kuyaenzi Mapinduzi matukufu ya Zanzibar.

2. Kujenga fikra mpya za kurejesha kujiamini na kufufua azma ya kujitegemea kama Taifa. Ni dhahiri kuwa pamoja na rasilimali zetu, bado Tanzania ni taifa tegemezi. Bado tunajidanganya kuwa wafadhili watatujengea nchi. Tukumbuke, nchi zinajengwa nawananchi wake. 
 
Nasi pia lazima tujikomboe kifkra na tuondokane na utamaduni wa kuwa tegemezi. Tuanze kwa kujipiga kifua kwa kujiamini kuwa tunaweza kujitegemea na kuijenga Tanzania sisi wenyewe.Kujiamini na kujitegemea ndio uhuru wa kweli.

3. Kujenga uzalendo, uadilifu ikiwa ni pamoja na kuimarisha uwazi katika shughuli zote za serikali na kupambana na rushwa.Watanzania tumepoteza uzalendo kwa kiasi kikubwa. Kuna vitendo vinavyoashiria kuwa hatuipendi tena nchi yetu. 
 
Tunashabikia wizi na rushwa. Inabidi turejee kwenye misingi ya taifa letu misingi ya uadilifu na uzalendo. Tukumbuke kuwa hatuwezi kujenga uchumi wa kisasa kama tutaruhusu rushwa ishamiri.
 
 Wawekezaji hawataleta mitaji yao kwa wingi kama rushwa itaendelea kutawala katika huduma serikali na wananchi hawawezi kupata huduma bora kama rushwa itaendelea kutawala. Ni lazima tuipinge rushwa kwa vitendo sio maneno.

4. Kujenga Serikali madhubuti, makini na yenye nidhamu inayoendeshwa kwa misingi ya sheria, uwazi na uwajibikaji.Maendeleo ya watu hayawezekani bila serikali kusimamiautekelezaji sera na miradi na kuleta ufanisi katika kutoa huduma na kusimamia maendeleo. Tumekuwa wepesi wa kutunga sera lakini wazito wa kuzitekeleza na kuzisimamia.


5. Kuleta msukumo mpya wa ushirikiano kati ya serikali na sekta binafsi katika ujenzi wa uchumi wa kisasa na unaojitegemea. Sekta binafsi ndiyo nyenzo ya uchumi imara. Inazalisha mali, ajira na kuchangia kwa kiasi kikubwa katika pato la taifa kwa kulipa kodi.
 
 Ilisekta hii itoe mchango unaotakiwa katika maendeleo ni lazima ifanye kazi na serikali kwa karibu. Tukumbuke, bila uchumi imarahakuna huduma bora!


6. Uwekezaji katika huduma za jamii. Elimu na afya bora, mazingira, makazi safi na maji salama ndiyo mihimili ya maendeleo ya watu.
 
 Hii inawezekana tu iwapo serikali itakuwa na sera na utashi wa kuutambua uboreshaji wa huduma za jamii kama ndiyo lengo kuu la maendeleo ya nchi. Serikali nitayoiongoza itahakikisha kuwa kila Mtanzania anapata elimu bora na inayogharamiwa na serikali kama mimi na wenzangu tulivyopata. 
 
Wakatitunazungumzia kuunganisha soko la ajira katika Afrika Mashariki, hatuna budi kurekebisha mfumo wetu wa elimu na kuuelekeza kwenye mafunzo ya ufundi na ustadi yanayowajenga wahitimu wetu kuwa wabunifu, wenye kujiamini, wenye uwezo kushindana katika soko la ajira na wa kujiajiri. Napenda kusisitiza kuwa elimu ndiyo muhimili wa maendeleo, ndiyo mkombozi wa kweli wa binadamu. Mimi ni mfano hai wa ukombozi wa elimu. 
 
Elimu ndiyoimenivusha kutoka kijijini kwetu Ngarash na kunipa upeo wa kitaifa. Mama akiwa na elimu atajua umuhimu wa kumpeleka mwanae shule, anapata lishe bora na chanjo stahili na kuwa anaishi katika mazingira safi. Elimu ndilo jibu la umaskini, maradhi na ujinga.Taifa lililo elimika ni taifa lenye maendeleo.
 
7. Kujenga uchumi shirikishi unaolenga kuondoa umaskini.Mkakati wa kuondoa umaskini Tanzania lazima ujikite kwenye nguzo za ushiriki wa kila Mtanzania katika uchumi wa taifa. 
 
Kwa misingi hii, tukiweza kupunguza umaskini, tutaweza pia kupunguzatofauti za kipato ambazo tukiziacha ziendelee kukua kwa kiasi cha sasa, zinaweza kuhatarisha utulivu na amani katika jamii yetu.Uchumi shirikishi ndio silaha dhidi ya umaskini.

8. Kuimarisha ulinzi wa nchi na usalama wa raia na ujirani mwema.Itakuwa nia yangu kuimarisha misingi iliyojengwa kulinda na kudumisha umoja na amani nchini. 
 
Kadhalika, nitahakikisha kuwa usalama wa mipaka ya Tanzania unaimarishwa kwa misingi ya ujirani mwema na kutanzua migogoro na matatatizo yoyote na nchi jirani, kwa njia ya diplomasia na mazungumzo.

Hitimisho:
Hii ndiyo misingi na dira ya uongozi wangu. Nachelea kusema kuwa haitakuwa kazi rahisi. Lakini kwa ushirikiano wa kila mmoja na maamuzi magumu, yote yanawezekana.
 
 Tumeona nchi nyingi zilizosimamiwa na utawala thabiti wa serikali za kimaendeleo zikikabili na kupunguza umaskini katika kizazi kimoja. Kama mataifa mengine yamefanikiwa, tena bila raslimali kama zetu, kwa nini sisi tushindwe? 
 
Tuna kila sababu ya kufanya maamuzi magumu sasa ili kuwajengea Watanzania matumaini mapya ya maendeleo. Naomba nisisitize kuwa katika uongozi wangu hakutakuwa na nafasi ya majungu, na visasi. Hatutaangalia nyuma bali tutasonga mbele kwani ndicho Watanzania wanakitarajiakutoka kwa uongozi uliojengwa kwenye misingi bora.

Ndugu Watanzania:-
Ni maono yangu kuwa siku si nyingi nchi yetu itaanza safari yenye uelekeo wa matumaini na neema tele kwa wananchi.

Ni maono yangu kuwa siku si nyingi sisi kama Watanzania kwa umoja wetu tutajivunia kuishi katika nchi tunayoipenda na inayoendeshwa kwa misingi ya utawala bora, chini ya serikali ya kimaendeleo iliyojengwa kwenye fikra mpya za uzalendo, uadilifu, utendaji na uwajibikaji.

Ni maono yangu kuwa Peke yangu sitaweza, lakini kwa maamuzi magumu na ushirikiano wa kila mmoja wetu ikiwa ni pamoja na wagombea wenzangu ndani ya CCM, inawezekana kuanza safari hii ya Matumaini Mapya.

Kabla ya kumaliza hotuba yangu hii fupi, kuna mambo matatu ningependa kuyaweka wazi hapa.

La kwanza, linahusu msingi wa uongozi ninaouamini na ambao nimeusema mara kadhaa hapa. Msingi huo ni UWAJIBIKAJI.Watanzania wananifahamu mimi si mtu wa maneno, ni mtu wa vitendo. Naamini kwa dhati kabisa kwamba huwezi kuwa na Uongozi imara utakaoweza kusimamia ujenzi wa Taifa imara iwapo huna ujasiri wa kuwajibika. Mimi nimeongoza kwa mfano, na pale ilipobidi, nilikubali kuwajibika na kubeba dhamana ya uongozinilipojiuzulu nafasi ya Waziri Mkuu.

La pili, mimi si mtu wa visasi. Siamini katika kuangalia ya nyuma. Yaliyopita si ndwele, tugange yajayo. Na kwa nini tuangalie nyuma wakati kama taifa tuna kazi kubwa sana mbele yetu inayohitaji kufanywa? Mimi ni Mkristo; najifunza kutoka kwa Bwana Yesu ambaye alipoulizwa: “Nisamehe mara ngapi?” Alijibu, “Samehe mara sabini mara saba”. Nitaenzi na kudumisha utamaduni huu wenye sura ya utu na heshima.

La Tatu, natambua kwamba dhamana ya Urais ni shughuli nzito hasa kwa taifa ambalo lina changamoto nyingi. Nataka niwahakikishie Watanzania wenzangu kwamba afya yangu ni njema kuweza kuwatumikia katika jukumu hili zito. Pamoja na vijineno vinavyosemwa pembeni, mimi mwenyewe ndiye ninayejijua zaidi. Nawahakikishia kuwa nisingekuja hapa leo na kueleza nia yangu hii ingekuwa sina uhakika na afya yangu.

Natoa RAI kwa Chama changu cha CCM, nadhani umefika wakati kwamba tutende tofauti na mazoea, watu wote walionyesha nia ya kutaka kuongoza, liundwe jopo la madaktari wa ndani na nje ya nchi tupimwe afya zetu, kwa hili najitolea kuwa wa KWANZA KUPIMWA afya yangu"
Laiti kama ungepata fursa ya kumwona Mhe.Lowassa baada ya hotuba hiyo ungemhoji swali gani?

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni