Pamoja na mambo mengine, kwa muda mrefu kumekuwa na sintofahamu kuhusu kipi ni kweli kuhusiana na Mhe.Lowassa na ufisadi wa RICHMOND. Kutokana na taarifa za awali kwamba Mhe.Edward Lowassa atatangaza nia leo, wadau wa habari, wachambuzi wa mambo ya kisiasa na wananchi wa kawaida walikuwa chonjo kutaka kujua kama ni kweli Mhe.Lowassa ataeleza ukweli kuhusu uhusika wake katika sakata la RICHMOND lakini jambo hilo hajalizungumzia kabisa.
![]() |
Mhe.Edward Lowassa (mwenye shati la kijani na mvi) akisalimiana na wapambe wake baada ya kutangaza nia rasmi katika uwanja wa Amri Abeid. |
Jisomee mwenyewe hapo chini sehemu ya hotuba yake uone kama kuna pahala amezungumzia sakata la RICHMOND au kuwa na lengo la kupiga vita ufisadi;
"Mimi, baada ya kutafakari kwa kina changamoto tulizo nazo na matarajio na matumaini waliyo nayo Watanzania, naamini kwamba Uongozi imara unaolenga kujenga Taifa imara unapaswa kuwa na dira yenye malengo yafuatayo:
-
Kuimarisha Muungano wetu kwa kuyashughulikia yanayotutenganisha na
kuyafanyia kazi ili yasivuruge yale yanayotuunganisha ambayo ni mengi
zaidi na makubwa zaidi.
-
Kushughulikia matumizi mabaya ya siasa za udini na ukabila kwa
kuimarisha siasa zilizoshiba uzalendo na zenye kutuelekeza kwenye
Utanzania wetu.
-
Kujenga uchumi imara na wa kisasa, na ambao ni shirikishi unaomnufaisha
kila Mtanzania aliyeko mjini au kijijini. Tunapaswa kubadili hali
tuliyo nayo sasa ambapo Kilimo kinaonekana kama kimesahauliwa na
wakulima wetu wanaonekana wanakata tamaa.
Wafugaji
na wavuvi nao wanahisi sekta zao hazijapewa umuhimu unaostahiki.
Tunahitaji kuondokana na hali iliyopo sasa ya kuwa Taifa linalouza
malighafi na badala yake kuwa Taifa linalosindika na kusarifu mazao na
kutengeneza wenyewe bidhaa zitokanazo na malighafi yake.
Ndani
ya miaka mitano ijayo tutahakikishatunaiondolea Tanzania sifa ya
kusafirisha malighafi na badala yake kusindika mazao yanayozalishwa hapa
nchini kama pamba, kahawa, chai na korosho na kuyaongezea thamani
(value addition).Mkakati huu utazalisha ajira nyingi na kuongeza mapato
ya fedha za kigeni nchini.
Tunahitaji
kujielekeza kwenye kujenga viwanda na kuleta ajira. Tuna vivutio vingi
sana vya utalii lakini bado Tanzania inapitwa na nchi kama Afrika Kusini
katika kuingiza idadi kubwa ya watalii.
Kwa
nini nchi kama Dubai iweze kuvutia watalii kwa mamilioni na Tanzania
tushindwe? Tunapaswa kukabiliana kikamilifu na hisia zilizopo miongoni
mwa wananchi kwamba Tanzania hainufaiki ipasavyo na utajiri wa
rasilimali zake nyingi ilizo nazo.
Tutajipanga zaidi kuhakikisha tunanufaika kama nchi na rasilimali zetu kama madini na gesi asilia. Hii ndio Safari ya Matumaini
-
Kukuza kipato cha wananchi na kunyanyua hali za maisha ya watu wetu.
Tunapaswa kuhakikisha kuwa ukuaji wa uchumi tunaouzungumzia unamnufaisha
Mtanzania aliyeko mjini au kijijini na kwamba hali za Watanzania wa
matabaka yote zinanyanyuka na kwamba wanaridhika na kuuona uhalisi wa
ukuaji wa maendeleo tunayoyazungumzia.
-
Kuondokana na sifa mbaya ya kuwa Taifa ombaomba. Kwa wingi wa
rasilimali tulizo nazo na neema ya ardhi, maziwa, mito na bahari
Tanzania tuna kila sababu ya kuacha kuwa ‘bakuli la ombaomba’ na badala
yake kuwa ‘mkoba wa neema’ katika Afrika.We can transform our nation
from being the begging bowl to become the bread basket of Africa.
-
Kujenga mfumo mpya wa elimu unaojielekeza kuwatayarisha vijana wetu
waweze kuajirika, kujiajiri na kushindana katika soko la ajira.
Tumepiga
hatua kadhaa katika elimu lakini kiwango cha elimu bado ni hafifu.
Pamoja na kuwa na shahada (degrees), bado wahitimu wetu hawawezi
kushindana kwenye soko la ajira.
Wakati
tunazungumzia kuunganisha soko la ajira katika Afrika Mashariki,hatuna
budi kujikita kubadili mfumo wetu wa elimu na kuuelekeza kwenye mafunzo
ya ufundi na stadi yanayowajenga wahitimu wetu kuwa wabunifu na wenye
kujiamini katika kukabiliana na changamoto za maendeleo duniani.
-
Kuhakikisha tunakabiliana ipasavyo na kulipunguza kwa kiasi kikubwa
kama si kulimaliza kabisa tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama.
Ni jambo la kusikitisha kwamba tumezungukwa na mito na maziwa lakini
bado watu wetu hawana maji ya kunywa hata ndani ya Dar es Salaam.
-
Kujenga na kusimamia mfumo imara wa kutekeleza sera na sheria
tunazozitunga na kuzipitisha kwa lengo la kumtumikia Mtanzania na
kumjengea uwezo wa kubadili maisha yake ili tuweze kwenda sambamba na
viwango vya kimataifa. Tanzania imepata sera na sheria nzuri sana lakini
utekelezaji wake umekuwa hafifu.
Tumekuwa
wepesi wa kutunga sera na sheria lakini wazito mno wa kuzitekeleza na
kuzisimamia. Uongozi imara wenye kulenga ujenzi wa Taifa imara
utahakikisha tunakuwa mfano wa utekelezaji wa sera na sheria tulizo nazo
na mpya zitakazotungwa kukabiliana na malengo tuliyojiwekea.
Mambo
haya niliyoyaeleza hapa ndiyo yatakayokuwa msingi mkuu wa utendaji wa
Serikali nitakayoiongoza pale nitakapopewa ridhaa ya kubeba bendera ya
CCM katika nafasi ya Urais na pia nitakapopewa ridhaa ya kuliongoza
Taifa letu kupitia uchaguzi mkuu wa mwaka huu.
Ramani ya Uongozi Imara Ninaouamini 9 Leadership Roadmap)
Kama
nilivyotangulia kusema, kazi ya kuongoza nchi si lelemama na hasa
unapoongozwa na dhamira ya dhati na msukumo wa ndani ya nafsi
unaojielekeza kubadilisha maisha ya wananchi wenzako waliokuamini
uwaongoze. Kwa vyovyote vile, hiyo haiwezi kuwa kazi ya mtu mmoja. Ni
kazi ya pamoja.
Lakini
ili muweze kufanya kazi kama timu moja iliyojipanga kisawasawa kuleta
mabadiliko yanayohitajika na ili muweze kweli kutoa Uongozi imara
unaojikita kujenga Taifa imara hapana budi kiongozi mkuu anayeongoza
timu hiyo aweke ramani anayokusudia kuifuata katika kutoa uongoziimara
anaoukusudia yaani ‘Leadership Roadmap’.
Pamoja
na kuwa sehemu ya uongozi huko nyuma, kutakuwa na maamuzi na matumaini
mapya. Ramani ya uongozi imaraninayokusudia kuutoa kwa wenzangu na
ambayo nitaitumia kuiongoza timu yangu katika kuwatumikia Watanzania wenzangu itajikita katika maeneo yafuatayo:
1.
Kurejea kwenye Katiba katika kuainisha nia, dhamira na malengo yetu ya
kujenga jamii inayozingatia misingi ya demokrasia, udugu na amani.
Muhimu katika hili ni kukemea tabia mbaya zinazochochea mfarakano katika
jamii kama vile matumizi mabaya ya siasa za udini na ukabila.
Aidha
moja ya misingi muhimu ya Katiba ni Muungano wetu. Itakuwa dhamira
yangu kuimarisha misingi ya Muungano pamoja na udugu wa damu nahistoria
ya ushirikiano iliyojengwa na waasisi wetu, Baba wa Taifa Mwalimu Julius
Kambarage Nyerere na Hayati Sheikh Amri Abeid Karume na kuyaenzi
Mapinduzi matukufu ya Zanzibar.
2.
Kujenga fikra mpya za kurejesha kujiamini na kufufua azma ya
kujitegemea kama Taifa. Ni dhahiri kuwa pamoja na rasilimali zetu, bado
Tanzania ni taifa tegemezi. Bado tunajidanganya kuwa wafadhili
watatujengea nchi. Tukumbuke, nchi zinajengwa nawananchi wake.
Nasi
pia lazima tujikomboe kifkra na tuondokane na utamaduni wa kuwa
tegemezi. Tuanze kwa kujipiga kifua kwa kujiamini kuwa tunaweza
kujitegemea na kuijenga Tanzania sisi wenyewe.Kujiamini na kujitegemea
ndio uhuru wa kweli.
3.
Kujenga uzalendo, uadilifu ikiwa ni pamoja na kuimarisha uwazi katika
shughuli zote za serikali na kupambana na rushwa.Watanzania tumepoteza
uzalendo kwa kiasi kikubwa. Kuna vitendo vinavyoashiria kuwa hatuipendi
tena nchi yetu.
Tunashabikia
wizi na rushwa. Inabidi turejee kwenye misingi ya taifa letu misingi ya
uadilifu na uzalendo. Tukumbuke kuwa hatuwezi kujenga uchumi wa kisasa
kama tutaruhusu rushwa ishamiri.
Wawekezaji
hawataleta mitaji yao kwa wingi kama rushwa itaendelea kutawala katika
huduma serikali na wananchi hawawezi kupata huduma bora kama rushwa
itaendelea kutawala. Ni lazima tuipinge rushwa kwa vitendo sio maneno.
4.
Kujenga Serikali madhubuti, makini na yenye nidhamu inayoendeshwa kwa
misingi ya sheria, uwazi na uwajibikaji.Maendeleo ya watu hayawezekani
bila serikali kusimamiautekelezaji sera na miradi na kuleta ufanisi
katika kutoa huduma na kusimamia maendeleo. Tumekuwa wepesi wa kutunga
sera lakini wazito wa kuzitekeleza na kuzisimamia.
5.
Kuleta msukumo mpya wa ushirikiano kati ya serikali na sekta binafsi
katika ujenzi wa uchumi wa kisasa na unaojitegemea. Sekta binafsi ndiyo
nyenzo ya uchumi imara. Inazalisha mali, ajira na kuchangia kwa kiasi
kikubwa katika pato la taifa kwa kulipa kodi.
Ilisekta
hii itoe mchango unaotakiwa katika maendeleo ni lazima ifanye kazi na
serikali kwa karibu. Tukumbuke, bila uchumi imarahakuna huduma bora!
6.
Uwekezaji katika huduma za jamii. Elimu na afya bora, mazingira, makazi
safi na maji salama ndiyo mihimili ya maendeleo ya watu.
Hii
inawezekana tu iwapo serikali itakuwa na sera na utashi wa kuutambua
uboreshaji wa huduma za jamii kama ndiyo lengo kuu la maendeleo ya nchi.
Serikali nitayoiongoza itahakikisha kuwa kila Mtanzania anapata elimu
bora na inayogharamiwa na serikali kama mimi na wenzangu tulivyopata.
Wakatitunazungumzia
kuunganisha soko la ajira katika Afrika Mashariki, hatuna budi
kurekebisha mfumo wetu wa elimu na kuuelekeza kwenye mafunzo ya ufundi
na ustadi yanayowajenga wahitimu wetu kuwa wabunifu, wenye kujiamini,
wenye uwezo kushindana katika soko la ajira na wa kujiajiri. Napenda
kusisitiza kuwa elimu ndiyo muhimili wa maendeleo, ndiyo mkombozi wa
kweli wa binadamu. Mimi ni mfano hai wa ukombozi wa elimu.
Elimu
ndiyoimenivusha kutoka kijijini kwetu Ngarash na kunipa upeo wa
kitaifa. Mama akiwa na elimu atajua umuhimu wa kumpeleka mwanae shule,
anapata lishe bora na chanjo stahili na kuwa anaishi katika mazingira
safi. Elimu ndilo jibu la umaskini, maradhi na ujinga.Taifa lililo
elimika ni taifa lenye maendeleo.
7.
Kujenga uchumi shirikishi unaolenga kuondoa umaskini.Mkakati wa kuondoa
umaskini Tanzania lazima ujikite kwenye nguzo za ushiriki wa kila
Mtanzania katika uchumi wa taifa.
Kwa
misingi hii, tukiweza kupunguza umaskini, tutaweza pia kupunguzatofauti
za kipato ambazo tukiziacha ziendelee kukua kwa kiasi cha sasa,
zinaweza kuhatarisha utulivu na amani katika jamii yetu.Uchumi
shirikishi ndio silaha dhidi ya umaskini.
8.
Kuimarisha ulinzi wa nchi na usalama wa raia na ujirani mwema.Itakuwa
nia yangu kuimarisha misingi iliyojengwa kulinda na kudumisha umoja na
amani nchini.
Kadhalika,
nitahakikisha kuwa usalama wa mipaka ya Tanzania unaimarishwa kwa
misingi ya ujirani mwema na kutanzua migogoro na matatatizo yoyote na
nchi jirani, kwa njia ya diplomasia na mazungumzo.
Hitimisho:
Hii
ndiyo misingi na dira ya uongozi wangu. Nachelea kusema kuwa haitakuwa
kazi rahisi. Lakini kwa ushirikiano wa kila mmoja na maamuzi magumu,
yote yanawezekana.
Tumeona
nchi nyingi zilizosimamiwa na utawala thabiti wa serikali za
kimaendeleo zikikabili na kupunguza umaskini katika kizazi kimoja. Kama
mataifa mengine yamefanikiwa, tena bila raslimali kama zetu, kwa nini
sisi tushindwe?
Tuna
kila sababu ya kufanya maamuzi magumu sasa ili kuwajengea Watanzania
matumaini mapya ya maendeleo. Naomba nisisitize kuwa katika uongozi
wangu hakutakuwa na nafasi ya majungu, na visasi. Hatutaangalia nyuma
bali tutasonga mbele kwani ndicho Watanzania wanakitarajiakutoka kwa
uongozi uliojengwa kwenye misingi bora.
Ndugu Watanzania:-
Ni maono yangu kuwa siku si nyingi nchi yetu itaanza safari yenye uelekeo wa matumaini na neema tele kwa wananchi.
Ni
maono yangu kuwa siku si nyingi sisi kama Watanzania kwa umoja wetu
tutajivunia kuishi katika nchi tunayoipenda na inayoendeshwa kwa misingi
ya utawala bora, chini ya serikali ya kimaendeleo iliyojengwa kwenye
fikra mpya za uzalendo, uadilifu, utendaji na uwajibikaji.
Ni
maono yangu kuwa Peke yangu sitaweza, lakini kwa maamuzi magumu na
ushirikiano wa kila mmoja wetu ikiwa ni pamoja na wagombea wenzangu
ndani ya CCM, inawezekana kuanza safari hii ya Matumaini Mapya.
Kabla ya kumaliza hotuba yangu hii fupi, kuna mambo matatu ningependa kuyaweka wazi hapa.
La
kwanza, linahusu msingi wa uongozi ninaouamini na ambao nimeusema mara
kadhaa hapa. Msingi huo ni UWAJIBIKAJI.Watanzania wananifahamu mimi si
mtu wa maneno, ni mtu wa vitendo. Naamini kwa dhati kabisa kwamba huwezi
kuwa na Uongozi imara utakaoweza kusimamia ujenzi wa Taifa imara iwapo
huna ujasiri wa kuwajibika. Mimi nimeongoza kwa mfano, na pale
ilipobidi, nilikubali kuwajibika na kubeba dhamana ya
uongozinilipojiuzulu nafasi ya Waziri Mkuu.
La
pili, mimi si mtu wa visasi. Siamini katika kuangalia ya nyuma.
Yaliyopita si ndwele, tugange yajayo. Na kwa nini tuangalie nyuma wakati
kama taifa tuna kazi kubwa sana mbele yetu inayohitaji kufanywa? Mimi
ni Mkristo; najifunza kutoka kwa Bwana Yesu ambaye alipoulizwa:
“Nisamehe mara ngapi?” Alijibu, “Samehe mara sabini mara saba”. Nitaenzi
na kudumisha utamaduni huu wenye sura ya utu na heshima.
La
Tatu, natambua kwamba dhamana ya Urais ni shughuli nzito hasa kwa taifa
ambalo lina changamoto nyingi. Nataka niwahakikishie Watanzania
wenzangu kwamba afya yangu ni njema kuweza kuwatumikia katika jukumu
hili zito. Pamoja na vijineno vinavyosemwa pembeni, mimi mwenyewe ndiye
ninayejijua zaidi. Nawahakikishia kuwa nisingekuja hapa leo na kueleza
nia yangu hii ingekuwa sina uhakika na afya yangu.
Natoa
RAI kwa Chama changu cha CCM, nadhani umefika wakati kwamba tutende
tofauti na mazoea, watu wote walionyesha nia ya kutaka kuongoza, liundwe
jopo la madaktari wa ndani na nje ya nchi tupimwe afya zetu, kwa hili
najitolea kuwa wa KWANZA KUPIMWA afya yangu"
Laiti kama ungepata fursa ya kumwona Mhe.Lowassa baada ya hotuba hiyo ungemhoji swali gani?
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni