Lebo

Ijumaa, 12 Juni 2015

Mhe.Wassira apigwa na bumbuazi mbio za Urais CCM


Mhe.Steven Wassira akinadi sera Kirumba, Mwanza


Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika Mhe. Steven Wassira amegeuka na kuwa mchekeshaji katika harakati za kuusaka Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM). Hii ni baada ya kutoa kauli yenye utata na ambayo imetafsiriwa kuwa ni kichekesho miongoni mwa wananchi waliofika kumsikiliza katika harakati zake za kuelekea ikulu.

Pamoja na mambo mengine ya msingi, Mhe.Wassira amesema anawashangaa wagombea wenzake kwa kutoa fedha wakilenga kununua uongozi wakati uongozi siyo biashara.
Wasira alitoa kauli hiyo jana wakati akiwashukuru wanachama wa CCM waliojitokeza kumdhamini katika Uwanja wa CCM Kirumba, kama sehemu ya utaratibu wa chama hicho kuelekea mchakato wa kumpata mgombea urais katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba, mwaka huu. 
 
“Jamani wakati wa kujaza watu kwenye viwanja bado haujafika, mikutano ya hadhara bado. Kwa hiyo si kwamba hatuwezi kujaza watu, tukitaka tunaweza, lakini wakati bado, utafika tutajaza watu."
 
“CCM na taifa kwa sasa vipo katika mazingira magumu kisiasa, rushwa sasa inainyemelea kwa kasi kubwa siasa, hii ni hatari sana, kamwe tusije kubali nchi yetu kuwekwa rehani na kundi la mafisadi. 
 
“Mtu ambaye anataka kuiweka rehani nchi kamwe hawezi kuwa na hoja, ndio sababu mmeanza kuona watu wanaishiwa hoja. Mtanzania yoyote yule anayetumia mabilioni kununua nchi mwisho wa siku ataiuza tu,” alisema Wasira huku wadhamini wake wakishangilia. 
 
Wasira alisema tatizo la rushwa katika siasa ni kubwa kiasi cha kuwafanya baadhi ya watu kuamini kuwa wanaweza kuinunua CCM. 
 
“Hivi nani kakutuma kuinunua CCM? Unainunua kwa niaba ya nani. Nchi yetu haipo sokoni, na wala hatujawahi kutangaza tenda ya kuuza nchi, sasa mabilioni kwenye siasa ya kazi gani?” alihoji. 
 
Aliwasihi Watanzania kuwa makini kwa sababu kuna kila dalili nchi inapelekwa sokoni na watu wachache wasio itakia mema. 
 
Kada huyo mkongwe wa CCM aliwataka Watanzania kujiuliza na kutafakari ni wapi mabilioni yanayotumika yanatoka, na kuongeza kuwa wanaotoa fedha hizo uwezo wao kifedha hauonekani katika kulipa kodi. 
 
Aliwataka wananchi kukataa kugeuzwa kuku wa kienyeji, ambapo alitoa mfano wa mtu anayetaka kuwakusanya kuku huwakusanya kwa kuwarushia mtama au pumba, nao hukimbilia kula bila hata kutaza nyuma au kufikiri. 
 
 “Kuna wenzetu ambao kwa malengo yao maovu wameamua kuwageuza wananchi na kuwafanya kuku wa kienyeji, wanakuja na fedha zao na wanazitumia kuwakusanya kwenye viwanja, wananchi kataeni, vinginevyo majuto ni mjukuu,” alisema. 
 
Tayari Wasira amekwishapata wadhamini katika mikoa 20, ikiwamo sita ya Tanzania Visiwani na jana alidhaminiwa katika mikoa ya Mwanza, Shinyanga na Geita. 
Kwa upande mwingine wagombea wengine ambao ni Januari Makamba na Edward Ngoyai Lowassa wametajwa kuwa lulu mikoani. 

Mhe.January Makamba akizungumza na wana CCM mkoani Iringa                                                                                                                                                                                  

Mhe. January Makamba ameripotiwa kujizolea wadhamini 600 mkoani Iringa ambapo mchakato maalumu ilibidi ufanyike ili kuwapata wawakilishi wachache.
Kwa upande wa Mhe. Lowassa ameripotiwa kung'ang'aniwa na wananchi mjini Shinyanga wote wakitaka kumuona.
Mhe.Edward Lowassa akisalimiana na wananchi mjini Shinyanga.

 
 Pamoja na mambo mengine, shughuli iliyonogesha safari ya Lowassa mjini Shinyanga ni pamoja na kitendo cha Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira) Mhe. Steven Maselle kutangaza kumuunga mkono Mhe.Lowassa. 
 
Duru za siasa kutoka vyanzo vya ndani ya CCM vinaeleza kuwa Mhe.Edward Lowassa yumo katika matazamio ya jina lake kukatwa mapema katika kinyang'anyiro hiki kutokana na kile kinachoelezwa kuwa matumizi mabaya ya fedha zake. Lakini hili laweza kuwa tetesi tu, maana siasa za CCM hujielekeza zaidi kwa mgombea mwenye kutabirika katika muktadha wa ushindi.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni