Lebo

Jumatano, 17 Juni 2015

Msajili wa vyama aonya matumizi makubwa kampeni za uchagu

Jaji Francis Mtungi akifunguja mkutano wa wadau wa siasa  wa uimatishaji demokrasia ya vyama vingi
Msajili wa vyama vya siasa nchini JAJI FRANCIS MUTUNGI


Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa imetoa tahadhari kwa wagombea watakaokiuka Sheria ya Gharama za Uchaguzi ya mwaka 2010 watakuwa wanajiweka katika hatari ya kutoteuliwa na vyama vyao.

Hadi sasa vyama ambavyo makada wake wameanza kuchukua fomu za kuomba kuwania urais ni Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha Wananchi (CUF).

Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi (pichani), alitoa tahadhari hiyo jana wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam kuhusu sheria ya gharama za uchaguzi na sheria ya vyama vya siasa ambazo zinapaswa kuzingatiwa na vyama na wanasiasa katika kipindi hiki kuelekea uchaguzi mkuu.

“Natoa tahadhari au angalizo kwa vyama vya siasa na wanasiasa wasipuuzie utii wa sheria ya gharama za uchaguzi kwa sababu kutawaathiri nje na ndani ya vyama ,” alisema.

Mutungi alisema katika kipindi cha kuelekea uchaguzi mkuu mgombea yeyote au chama cha siasa asipozingatia sheria hiyo atakuwa anahatarisha nafasi yake ya kugombea na kutoteuliwa na chama chake kutokana na kukiuka masharti yaliyopo ndani ya sheria hiyo.

Alisema chama cha siasa kitakachopuuzia sheria ya uchaguzi na kikapitisha mgombea ambaye amekiuka masharti yaliyomo ndani ya sheria hiyo kitakuwa kinapitisha mgombea ambaye atawekewa pingamizi na atakuwa amejiharibia nafasi hiyo.

“Sitaki kuamini kuwa sekretarieti ya chama kilichosajiliwa kisizingatie utii wa sheria ya uchaguzi, kila mtu ni jukumu lake kuzingatia utii wa sehria bila shututi,” alisema.

Jaji Mutungi alisema kipindi hiki siyo muda mwafaka wa kufanya tathmini kama vyama vya siasa na wagombea wamezingatia sheria hiyo kwani hivi sasa ofisi ya msajili na vyombo vingine vinaendelea kufuatilia suala hilo na muda ukifika matokeo yatatolewa kwa kuweka wazi vyama na wagombea waliokiuka sheria.

Aliongeza kuwa sheria ya gharama za uchaguzi madhumuni yake yaliwekwa kwa misingi ya kutaka kudhibiti matumizi ya gharama katika mchakato wa uchaguzi na kuthibiti vitendo vinavyokataza na sheria ya nchi.

“Vyama vya siasa vinapaswa kufahamu kuna mambo ambayo sheria inakataza ikiwamo kufanya malipo kwa wapigakura ili kumchagua mgombea fulani, kuahidi kazi ama cheo, kutoa mikopo na ahadi ama makubaliano yoyote kwa mpiga kura ili kumchagua mgombea,” alisema.

Sheria ya gharama za uchaguzi imeainisha wazi kuwa chama cha siasa ndicho kitagharamia mchakato wa kura ya maoni na kampeni za uchaguzi ikiwa ni pamoja na gharama zote zitakazotumika kwa ajili ya uhamasisahaji kwa lengo la kumnadi mgombea kwa wapiga kura.

Pia sheria hiyo inaelekeza kuwapo kwa uwazi katika mapato na matumizi ya vyama na wagombea wao kabla na baada ya uchaguzi.

Sheria ya Gharama za Uchaguzi ilitungwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika mkutano wake wa 18, uliofanyika Januari 2010.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni