Lebo

Ijumaa, 3 Julai 2015

KAMBI YA WAKIMBIZI YA NYARUGUSU IMEZIDIWA



Kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu mkoani Kigoma, imeelemewa baada ya idadi ya wakimbizi kutoka Burundi kuzidi kuongezeka hivyo kuzidi uwezo wake kama inavyotakiwa na sheria za Umoja wa Mataifa (UN).
Mkurugenzi Idara ya Wakimbizi, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Harrison Mseke, alisema bado wakimbizi wa Burundi hawajaanza kurudi nyumbani kwao bali hali imekuwa mbaya zaidi kutokana na idadi yao kuendelea kuongozeka.
Kwa mujibu wa Mseke, hadi sasa wakimbizi katika kambi hiyo kutoka Burundi, wamefikia 71,000 na ndani ya wiki moja iliyopita wameingia wakimbizi 10,000.
Alisema kwa sasa idadi ya wakimbizi wote kutoka Burundi na nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), katika kambi hiyo ni takribani 100,000.
Kwa mujibu wa mkurugenzi huyo, idadi hiyo ni kubwa kupita kiasi kwani sheria za UN kupitia shirika lake la kuhudumia wakimbizi duniani (UNHCR) kambi moja inapaswa kuhudumia wakimbizi wasiozidi 50,000.

“Kuna tatizo kubwa la eneo la kuwaweka kwani wakimbizi wote kutoka Burundi na DRC, bado wanahifadhiwa  katika kambi ya  Nyarugusu. Kwa sheria za Umoja wa Mataifa, kambi moja inatakiwa kuwa na wakimbizi 50,000, lakini sasa wapo zaidi ya 100,000.
Mseke, alisema hadi sasa serikali inafanya utaratibu wa kujenga kambi nyingine ili kupunguza idadi hiyo na kuangalia uwezekano wa kuwatenganisha wakimbizi hao kutoka nchi hizo.
Ongezeko la wakimbizi kutoka Burundi, limechangiwa na vurugu za kisiasa zinazoendelea nchini humo baada ya Rais wake, Pierre Nkurunzinza, kutangaza kuwania urais kwa kipindi kingine cha tatu hivyo kudaiwa kukiuka katiba ya taifa hilo.
SOURCE:Nipashe

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni